TRA YAKEMEA WANAOINGIZA MAGENDO, WASIOTUMIA EFD

Mkuu wa Wilaya ya Kigoma Rashid Chuachua (katikati) aliyekuwa mgeni rasmi katika Siku ya Shukrani kwa Mlipa Kodi mkoani Kigoma, kulia ni Meneja wa TRA mkoa wa Kigoma Beatus Nchota na kushoto ni Kamishina wa Forodha na Ushuru wa Bidhaa Bi Julieth Nyamolelo aliyemwakilisha Kamishina Mkuu wa TRA.
Na Fadhili Abdallah, Kigoma
MAMLAKA ya mapato nchini (TRA) imesema kuwa uingizaji wa bidhaa nchini bila kulipiwa kodi zinazostahili (bidhaa za magendo) imekuwa changamoto kubwa ambayo inavuruga malengo ya mamlaka hiyo katika kufikia lengo la ukusanyaji kodi nchini.
Naibu Kamishna wa forodha na ushuru wa bidhaa TRA Makao Makuu, Julieth Nyomolelo amesema hayo katika haflaya utoaji zawadi kwa walipa kodi waliofanya vizuri kwa mwaka 2023/2024 kwa wafanyabiashara na wasafirishaji wa bidhaa wa mkoa Kigoma tuzo zinazolenga kuwatambua na kuwatia moyo wafanyabiashara wanaolipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
Nyomolelo akizungumza katika hafla hiyo amesema kuwa ulipaji kodi kwa hiari kwa kufuata taratibu za kisheria kulingana na biashara iliyofanyika inatija kubwa katika kuongeza makusanyo ya mamlaka hiyo sambamba na kufikia au kuvuka lengo lililoweka hivyo ametoa wito kwa watu wote kufuata taratibu na kulipa kodi kwa hiari na kwa wakati.
Awali Meneja wa TRA mkoa Kigoma,Beatus Mchota amesema kuwa Pamoja na changamoto ya uingizaji bidhaa kwa njia ya magendo kuvuruga malengo yao pia wafanyabiashara wasiotumia mashine za kielektorniki wameongeza changamoto kubwa katika suala la ukadiriaji na ulipaji kodi kwa hiari kwani sehemu kubwa ya mauzo yao yanakuwa hayaingii kwenye hesabu za biashara waliyofanya.
Akizungumza katika hafla hiyo Mkuu wa wilaya Kigoma,Dk.Rashid Chuachua ambaye alimwakilisha Mkuu wa mkoa Kigoma,Thobias Andengenye amesema kuwa anaipongeza TRA kwa kazi kubwa ya kukusanya kodi na kufikia malengo ya ukusanyaji yaliyowekwa jambo ambalo linaifanya serikali kuweka mazingira wezeshi ya kuifanya mamlaka hiyo kutimiza malengo yake kwa ufanisi.
Chuachua amesema kuwa kuongezeka kwa makusanyo ya kodi kunaakofanywa na TRA kumeifanya serikali kutekeleza miradi mikubwa Kwenda kwa wananchi hivyo ametoa wito kwa wafanyabiashara kutojihusisha na biashara na magendo kwani licha ya kuinyima mapato serikali laakini pia kunasababisha kuingiza bidhaa ambazo hazina viwango na hatari kwa afya.

Naibu Kamishna wa forodha na ushuru wa bidhaa TRA Makao makuu Julieth Nyomolelo (kulia) akikabidhi tuzo kwa mfanyabiashara wa mkoa Kigoma Kilahumba Kivumo (kushoto) ambaye amekuwa mmoja wa wafanyabiashara waliofanya vizuri mkoani Kigoma.
Mmoja wa wafanyabiashara waliopewa tuzo kwenye hafla hiyo, Kilahumba Kivumo amesema kuwa mabadiliko ya utendaji ya maafisa wa TRA ambayo yametokana na vikao vya mara kwa mara wanavyofanya imekuwa chachu kwa wafanyabishara kulipa kodi kwa hiari na kuwaita maafisa hao kuwapa ushauri badala ya kuwakimbia.

Sehemu ya wafanyabiashara na wageni waliohudhuria utoaji tuzo kwa wafanyabiashara wa mkoa Kigoma waliofanya vizuri katika ulipaji kodi